Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, ujumbe wa Kiongozi Mkuu wa Mapinduzi ya Kiislamu ni kama ifuatavyo:
Kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, Mwenye Kurehemu
Wiki ya kwanza ya mwezi wa Shahrivar ya kila mwaka ni fursa ya kuzungumzia huduma zinazotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Mwaka huu, Serikali ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imepata heshima ya kukutana kwa Wiki ya Serikali na siku za mazazi ya furaha na yenye baraka ya vizazi wawili vya mwezi wa Rabiul-Awwal, rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao na juu ya Ahlul-Bayt wao.
Katika fursa hii, nawapongeza na kuwaambia “Mungu awape nguvu” wafanyakazi wote na viongozi wanaofanya kazi kwa bidii katika taasisi za Serikali, na hususan Rais mkweli na mwenye kujali wa Serikali ya Awamu ya Kumi na Nne. Hasa kwa kuzingatia hatua zinazostahili ambazo, licha ya vikwazo na njama mbalimbali za adui wa Marekani na Uzayuni, pamoja na kuongezeka kwa vikwazo na mizingiro, zimechukuliwa wakati wa vita vya tatu vya kulazimishwa na baada yake, katika njia ya kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa na aina mbalimbali za huduma zinazohitajika na wananchi, kurekebisha maeneo muhimu yaliyoharibiwa, na kusimamia nishati.
Vilevile, inafaa tukawakumbuka kwa heshima Marais mashahidi Rajai na Raisi, Waziri Mkuu shahidi Bahonar, pamoja na wafanyakazi, viongozi na mawaziri mashahidi katika vipindi mbalimbali vya Serikali; na juu ya wote, tumkumbuke kwa heshima Kiongozi Mkuu wa Mapinduzi aliyekuwa shahidi, ambaye alishikilia nafasi ya Urais wa Jamhuri kwa kipindi cha karibu mihula miwili. Tuwaombee wote daraja za juu na neema za Mwenyezi Mungu.
Fursa ya kuwahudumia wananchi na kutumikia malengo ya Jamhuri ya Kiislamu ni neema yenye thamani ambayo inapaswa kulindwa na kuthaminiwa. Katika zama hizi na hali nyeti na changamano ambayo lengo la kuifikisha “Iran yenye nguvu zaidi na zaidi” linakabiliana nayo, moja ya mambo muhimu ya kufikia lengo hili, sambamba na juhudi za mchana na usiku na ubunifu endelevu, ni kueleza na kusimulia nguvu na uwezo wa Iran na taifa lake pendwa, na kuviweka wazi zaidi.
Udhaifu na mapungufu havihitaji kusimuliwa na kupewa umaarufu; bali inahitaji mipango na hatua za kuondoa na kutatua matatizo hayo. Wakati mwingine, kueleza kwa uaminifu udhaifu wetu katika wakati ambao adui anahitaji kupata nguvu ya kisaikolojia, ni msaada mkubwa kwake; na huenda pia kukasababisha nyoyo za marafiki na wale wanaotuunga mkono kuwa na wasiwasi, na kuwafanya wachanganyikiwe na kutokuwa na uhakika. Naam, pale wasikilizaji wa kauli hizi za ukweli wanapokuwa ni wananchi wetu na watu wanaotujali pekee, tatizo hupungua. Lakini nguvu, uwezo na mambo mazuri, kwa mujibu wa mafundisho ya Qur’ani ya «وَأَمَّا بِنِعْمَةِ رَبِّكَ فَحَدِّثْ» — “ Na kuhusu neema ya Mola wako, itaje” — yanahitaji kusimuliwa na kuwekwa wazi zaidi.
Wananchi wapendwa wa Iran, ambao katika kipindi cha miezi sita iliyopita wameoyesha kiwango chao halisi katika nyanja mbalimbali za jihadi dhidi ya adui, uwepo wao katika medani, mshikamano, umoja wa nyoyo na ushirikiano wao, wanastahili na wana haki ya kuhisi kwamba huduma zinazotolewa na mihimili ya Serikali na taasisi zinazohusika ndani ya Jamhuri ya Kiislamu ziko katika njia ya kuifikisha nchi katika kiwango kinachostahili mfumo huu mtukufu na hadhi ya juu ya taifa lililotumwa.
Bila shaka, yale yatakayotajwa hapa chini yapo katika kiini cha mipango ya Serikali inayohudumia wananchi au, kwa namna fulani, yamo katika orodha ya malengo yake; na kuyataja hapa ni kwa ajili ya kukumbushia tu.
Miongoni mwa mambo hayo ni umuhimu wa kuzingatia kwa dhati mlolongo wa changamoto za kiuchumi na maisha ya wananchi, kama vile mfumuko wa bei, ukosefu wa ajira, usimamizi wa bei na soko la bidhaa na huduma, pamoja na kutoa kipaumbele maalumu kwa baadhi ya vipengele vingine vya uchumi, kama vile ukuaji, kuongeza uwekezaji na kuupeleka katika maeneo yenye manufaa na mahitaji, kukuza uzalishaji, kuondoa hatua kwa hatua dola ya Marekani katika nafasi yake muhimu ya kushiriki katika uchumi, na hatimaye kuweka mkusanyiko wa sera za uchumi wa kujitegemea na wenye kustahimili misukosuko kuwa mhimili mkuu.
Ufunguo mkuu katika eneo hili wa kutatua mambo yote haya unaonekana katika kaulimbiu ya kutegemea zaidi uzalishaji wa ndani. Bila shaka, kuhakikisha uwepo wa kiwango cha kutosha cha bidhaa za umma na bidhaa maalumu ni jambo la lazima kabisa. Kwa kuzingatia hilo, pale ambapo uzalishaji wa ndani hautoshelezi mahitaji, inapaswa kunufaika na uagizaji wa bidhaa kutoka nje kwa njia sahihi na yenye hekima.
Kwa kawaida, kuhamasisha uzalishaji, huku wakati huo huo kukisimamiwa uagizaji wa bidhaa kutoka nje na bei, kunaweza kusababisha hali ambayo madoa meusi yanayoonekana katika ukurasa wa uchumi wa nchi yataanza kupungua hatua kwa hatua, hadi hatimaye yatoweke kabisa.
Katika uwanja huu, ingawa mwenendo wa adui wakati wa vita na baada yake hauna athari ndogo, lakini usimamizi wenye hekima zaidi wa vipengele mbalimbali vya eneo hili, pamoja na kuomba msaada katika baadhi ya mambo kutoka kwa wananchi na katika mambo mengine kutoka kwa wataalamu na wabunifu wa teknolojia, na kugeuza uwezo mpya kuwa vitendo, kutaipeleka nchi kuelekea kupanuka kwa mambo ya maendeleo na ustawi.
Adui aliyeapa dhidi ya taifa hili anajaribu kuaminisha watu kwamba njia ya ujenzi na maendeleo inapitia katika kumfuata yeye na kutekeleza matakwa yake yasiyo na msingi; wakati ambapo kuchunguza yale aliyolifanyia taifa hili na rasilimali zake katika vipindi vya nyuma, hata miaka mingi kabla ya Mapinduzi ya Kiislamu, kunaonesha kinyume cha jambo hilo.
Miongoni mwa masuala na mada nyingine muhimu ni kutumia teknolojia na ubunifu unaopendekezwa na vijana wasomi. Wakati mwingine, kutumia kwa wakati mwafaka fursa hii na kuacha taratibu za kawaida pamoja na mazoea yaliyozoeleka katika jambo fulani kunaweza kuleta hatua kubwa na yenye ufanisi katika njia ya maendeleo na ustawi wa nchi.
Jambo hili linaweza kufikiriwa katika matawi mbalimbali ya uzalishaji wa nguvu, yakiwemo kilimo, viwanda, utamaduni na malezi, pamoja na masuala ya mawasiliano na kijamii.
Na miongoni mwa masuala ya msingi ya nchi ambayo daima yanapaswa kuwa katikati ya uangalizi wa Serikali na viongozi wa Serikali, pamoja na maafisa wote na mihimili yote ya utawala, ni kuheshimu umoja na kulinda mshikamano wa kijamii.
Kila hatua katika kila moja ya nyanja kuu za utamaduni, jamii, siasa, usalama na uchumi inapaswa kuchukuliwa kwa kuzingatia kiambatisho kinachohusiana na mshikamano wa kijamii.
Baadhi ya hatua ambazo kwa mtazamo wa nje zinaweza hata kuwa na wafuasi miongoni mwa baadhi ya makundi ya wananchi, ikiwa hazina kiambatisho hicho, au kile kilichoandaliwa kama kiambatisho hakizingatiwi katika utekelezaji, zinaweza kusababisha madhara kwa makundi hayo hayo na kwa wengine.
Bila shaka, kila kauli inayokatisha tamaa na kudhoofisha hamasa za kitaifa na za umma, pamoja na kila aina ya kuunda migawanyiko ya kufikirika kama vile vita au mazungumzo, maridhiano au misimamo mikali, suluhu au uchochezi wa vita, ambayo hapo nyuma imewasababishia wananchi wetu wapendwa hasara za moja kwa moja au zisizo za moja kwa moja, inaweza kuleta athari hiyo hiyo kuanzia sasa.
Kwa hiyo, ninatangaza kwa uthabiti kwamba kufanya jambo lolote linalodhuru mshikamano wa kijamii ni marufuku. Na miongoni mwa masuala mengine muhimu ni kutoa kipaumbele cha kimkakati kupita mipaka kwa suala la utamaduni, elimu na malezi.
Usemi “kimkakati kupita mipaka” unamaanisha kwamba uundaji wa mikakati mingine unapaswa kufanywa kwa kuzingatia suala hili. Katika nafasi hii, kuzingatia makundi ambayo ni chanzo cha kueneza utamaduni chanya na wenye kujenga, kama vile walimu katika elimu ya msingi na sekondari, vyuo vikuu na Hawzah, pamoja na wauguzi na madaktari ambao wamejitolea wenyewe kutekeleza wajibu wao katika taasisi zisizo za kibinafsi, kuna umuhimu wa pekee.
Vilevile, kuzingatia nafasi ya wanawake wanaobaki majumbani, ambao ni walimu wa watoto wa nchi hii, ndani ya mipaka ya nyumba, kwa kuwafundisha vipengele nyeti zaidi vya mchoro wa utamaduni mzuri na unaotakiwa wa siku zijazo, pia kuna umuhimu wa aina hiyo.
Tunatumaini kwamba kutekeleza mambo haya na mambo mengine yenye manufaa ambayo, kwa rehema za Mwenyezi Mungu, yanaweza kupatikana katika orodha ya mipango ya Serikali, kutaielekeza nchi yetu pendwa kuelekea “Iran yenye nguvu zaidi na zaidi”, na kuwafanya wanaoshiriki katika njia hii kustahiki uangalizi maalumu wa Imam wa zama (ajt), pamoja na dua zao njema, baraka na uongofu.
Wassalaamu ‘alaykum warahmatullaahi wabarakaatuh.
Sayyid Mojtaba Husseini Khamenei
6/Shahrivar/1405
Maoni yako